Na mwandishi wetu
Mfanyabiashara maarufu ambaye pia aliwahi kuwa mfadhili wa klabu ya soka yaYanga, Yusuf Manji amefariki dunia jana Jumamosi wakati akipatiwa matibabu nchini Marekani.
Mbali na kuwa mfadhili, Manji pia aliwahi kuwa kiongozi wa Yanga ambapo alijitahidi kuipa hadhi klabu hiyo kwa kufanya usajili wa wachezaji wa ndani na nje ya nchi wenye uwezo kwa lengo la kuipatia mafanikio timu hiyo.
Miongoni mwa wachezaji wa ndani ambao usajili wao ulitokana na juhudi za Manji ni wa kipa wa muda mrefu aliyejipatia mafanikio akiwa na klabu ya Simba, Juma Kaseja ambaye alisajiliwa Yanga ingawa hakudumu sana na timu hiyo.
Kupitia kampuni yake ya Quality Group Limited, Manji ambaye alikuwa bilionea aliiwezesha timu hiyo kutawala soka la ndani ingawa ufadhili wake haukuweza kuipa mafanikio timu hiyo katika michuano ya klabu barani Afrika.
Manji ambaye pia aliwekeza katika biashara ya magari hata hivyo aliingia katika mzozo na serikali hadi kufikia hatua ya kukamatwa na kuwekwa ndani kwa makosa mbalimbali yakiwamo madai ya kutolipa kodi.
Mara baada ya kuachiwa biashara nyingi za Manji zilianza kudorora na katika kipindi hicho akawa anaishi zaidi nje ya Tanzania kabla ya kuja mara chache lakini hakuweza kurudi katika hadhi yake ya zamani.
Taarifa kuhusu kifo cha bilionea huyo hata hivyo hazikuweka wazi maradhi yaliyokuwa yakimsibu hadi kufariki dunia na pia haijaelezwa mazishi yake yatafanyika lini na wapi.
Soka Manji afariki dunia
Manji afariki dunia
Read also