Na mwandishi wetu
Shirikisho la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (Cecafa), limetangaza rasmi michuano ya Kombe la Kagame 2024 itafanyika Tanzania Bara na Zanzibar kuanzia Julai 6 hadi 22 mwaka huu ikizishirikisha timu 16.
Awali, michuano hiyo ilipangwa kuanza Julai 20 hadi Agosti 4, mwaka huu, lakini kutokana na ratiba ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kuonesha kuanza Agosti, Cecafa wameamua michuano yao ianze mapema.
Lengo la Cecafa ni kuhakikisha michuano hiyo inamalizika siku chache kabla ya kuanza kwa mtifuano wa michuano ya CAF ngazi ya klabu msimu wa 2024/2025.
“Mashindano haya yatasaidia timu zetu katika ukanda huu kujiandaa vizuri kabla ya msimu wa CAF Champions League na CAF Confederation Cup 2024-2025 ambao unaanza mwezi Agosti.
“Na kuwa na timu kubwa kutoka DR Congo, Malawi na Zambia pia kunaibua msisimko kwenye mashindano yetu na kutoa changamoto halisi kwa timu zetu,” alisema leo Jumanne, Mkurugenzi Mtendaji wa Cecafa, John Gecheo.
Kulingana na hayo, michuano ya Cecafa Senior Challenge Cup 2024 ambayo yanahusisha timu za taifa iliyokuwa imepangwa kuanza Juni 29 mpaka Julai 14, mwaka huu, imeondolewa ili kuwapa wachezaji muda zaidi wa kujiandaa na klabu zao kabla ya Cecafa Kagame Cup.
Timu zitakazoshiriki michuano ya Cecafa Kagame Cup ni Vital’O ya Burundi, APR (Rwanda), El Merreikh, Al Hilal, Hai El Wadi (Sudan), Yanga, Simba, Azam, Coastal Union (Tanzania), Gor Mahia (Kenya), SC Villa (Uganda), JKU SC (Zanzibar), El Merreikh (Sudan Kusini).
Timu tatu nyingine zilizoalikwa kukamilisha idadi ya timu 16 katika mtanange huo ni Nyasa Big Bullets (Malawi), TP Mazembe (DR Congo) na Red Arrows (Zambia).
Kimataifa Kagame Cup kutimua vumbi Julai 6
Kagame Cup kutimua vumbi Julai 6
Read also