Na mwandishi wetu
Kaimu kocha mkuu wa Simba, Juma Mgunda amesema miongoni mwa mambo yaliyowaangusha kwenye sare ya bao 1-1 dhidi ya Kagera Sugar ni kutotumia vyema nafasi nyingi za kufunga walizozitengeneza.
Sare hiyo iliyopatikana Jumapili kwenye mechi hiyo iliyopigwa Uwanja wa Kaitaba, inakuwa sare ya pili kwa Mgunda katika mechi alizoiongoza timu hiyo hadi sasa huku akiwa ameshinda mechi tatu ambapo amesisitiza watapambana kuhakikisha makosa hayo ya kutotumia nafasi hayajirudii katika mechi zinazofuata.
“Matokeo ya sare hayamaanishi kwamba tumekwama ila haya ni mashindano, tumetengeneza nafasi nyingi lakini haikuwa riziki yetu, haikuwa bahati yetu, nafikiri ingekuwa habari nyingine kama ingekuwa ya kwetu leo lakini ndivyo mambo ya soka yalivyo.
“Iko wazi kuwa si kila nafasi mnayotengeneza mnaweza kufunga, tumetengeneza nafasi nyingi za kufunga lakini huo ndio mpira na ni sehemu ya mapungufu tuliyoyaona kwa hiyo sasa ni nafasi yetu kwenda kuyafanyia kazi kwa ajili ya kuhakikisha kwenye mechi zinazokuja kwamba tukipata nafasi tuzitumie vizuri na zitupe matokeo mazuri,” alisema Mgunda.
Matokeo ya sare yameifanya Simba iendelee kusalia nafasi ya tatu kwa pointi 57 ikiendelea kuifukuzia Azam iliyo nafasi ya pili kwa pointi 60 baada ya kushinda kwa mabao 2-1 dhidi ya KMC Jumapili.