Na mwandishi wetu
Bao la Clement Mzize limeiwezesha Yanga kutoka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Coastla Union na kutoka na pointi tatu katika mechi ya Ligi Kuu NBC iliyopigwa leo Jumatano kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.
Mzize ambaye aliingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Kennedy Musonda, alifunga bao hilo kwa kichwa katika dakika ya 70 akimalizia krosi iliyochongwa na Jesus Moloko aliyeinasa pasi ya Maxi Nzengeli.
Coastal ambao waliingia katika mechi hiyo kwa kujiamini waliidhibiti vizuri Yanga kwa kipindi cha kwanza wakifanya mashambulizi machache lakini walikuwa makini kuhakikisha Yanga hawapenyi katika lango lao.
Yanga ambao bado wana furaha ya ushindi wa mabao 5-1 walioupata dhidi ya Simba Jumapili, walipata wakati mgumu kuipenya safu ya ulinzi ya Coastal licha ya mashambulizi ya kila mara yaliyoongozwa na Pacome Zouazoa, Aziz Ki na wengineo ambao mashuti yao yaliokolewa na mlinda mlango wa Coastal, Matimba.
Katika dakika ya 63, Aziz Ki akiwa eneo lake la kujidai alichezewa rafu na Ibrahim Ajib wakati akijiandaa kufumua shuti na mwamuzi kuipa Yanga mpira wa adhabu ambao aliupiga Ki lakini haukuwa na madhara kwa Coastal.
Kwa ushindi huo Yanga imeendelea kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo ikiwa imefikisha pointi 24 katika mechi tisa na hadi sasa imepoteza mechi moja tu.
Soka Mzize aiadhibu Coastal Union
Mzize aiadhibu Coastal Union
Read also