Paris, Ufaransa
Mshambuliaji wa Inter Miami FC ya Marekani, Lionel Messi amesema anadhani anatakiwa kupewa nafasi ya kuaga rasmi katika timu yake ya zamani ya Barcelona katika tukio ambalo angependa liambatane na mechi maalum.
Tangu aondoke Barca Agosti 2021 na kujiunga na PSG ya Ufaransa akiwa mchezaji huru, kumekuwa na mazungumzo ya mchezaji huyo kuandaliwa mechi maalum ya kumpa heshima mchezaji huyo.
Mechi ya mwisho ya Messi akiwa na Barca ilikuwa Mei, 2021 dhidi ya Celta Vigo, mechi ambayo Barca ililala kwa mabao 2-1 lakini haikuwa na mashabiki kutokana na uwapo wa janga la Covid-19.
“Ningependa niwe na nafasi ya kuaga watu katika namna tofauti,” alisema Messi wakati akikabidhiwa tuzo ya Ballon d’Or, Jumatatu usiku jijini Paris, Ufaransa.
“Nafikiri kulikuwa na hali isiyopendeza wakati naondoka pale, si jambo zuri kwa mambo ambayo tulishirikiana nikiwa pale na kuishi pamoja, ninatakiwa kupata nafasi ya kuwaaga watu, Barcelona ni nyumbani, naipenda klabu na watu wa pale, kama kutakuwa na mechi maalum ningependa kuwa pale,” alisema Messi.
Messi ambaye ana rekodi ya kuifungia Barca mabao mengi, amekuwa na klabu hiyo kwa miaka 20 na kushinda jumla ya mataji 35 lakini kubwa zaidi ni.pale alipoiwezesha timu ya taifa ya Argentina kubeba Kombe la Dunia mwaka jana katika fainali zilizofanyika Qatar.
Mkurugenzi wa michezo wa Barca, Deco hivi karibuni alisema kwamba Messi atacheza mechi maalum ya kumuaga wakati rais wa klabu hiyo, Joan Laporta aliwahi kusema kwamba itapendeza Messi akiagwa rasmi katika mechi maalum ya kuumzindua uwanja mpya wa Nou Camp katika msimu wa 2025-26.
Naye mkurugenzi na mmiliki wa klabu ya sasa ya Messi ya Inter Miami, Jorge Mas alisema kwamba anaamini ni muhimu kwa Messi kupewa nafasi ya kuwaaga mashabiki wa Barca.
Kimataifa Messi atamani kuagwa rasmi Barca
Messi atamani kuagwa rasmi Barca
Read also