Na mwandishi wetu
Hatimaye timu ya JKT Tanzania imeeleza kuwa kwa sasa kuutumia Uwanja wa Azam Complex uliopo Chamazi, Dar es Salaam kwa ajili ya mechi zao za nyumbani za Ligi Kuu NBC.
Hayo yameelezwa Jumanne hii na Ofisa Habari wa JKT, Masau Bwire baada ya awali uwanja wao wa nyumbani wa CCM Kambarage uliopo Shinyanga kufungiwa na Bodi ya Ligi kwa kukosa vigezo baada ya kutumika kwenye mechi mbili za ligi pekee.
“Tulipokea barua Oktoba 3, mwaka huu juu ya kufungwa kwa uwanja wetu kutokana na kukosa vigezo vilivyoelezwa katika muonekano kwa watazamaji, eneo la kuchezea na sehemu nyingine, sasa uwanja uko kwenye matengenezo kwa hiyo tumechagua uwanja wetu wa nyumbani kama tulivyoelekezwa.
“Na chaguo la timu limekuwa Uwanja wa Azam Complex na tayari ratiba imepangwa na inaonesha hivyo kwamba tutatumia uwanja huo wakati huu ambao Kambarage sasa upo kwenye matengenezo na marekebisho kulingana na namna ilivyoelekezwa,” alisema Bwire.
Katika mechi mbili ilizocheza Uwanja wa Kambarage, JKT ilipata sare ya bao 1-1 dhidi ya Kagera Sugar kabla ya kuichapa Mashujaa bao 1-0.
Timu hiyo ambayo ipo nafasi ya saba kwenye msimamo wa ligi hiyo ikiwa na pointi saba, pia ilipata ushindi katika mechi na Namungo.